m

"If you want to conquer fear, don't sit at home and think about it. Go out and get busy. "

-- Dale Carnegie, motivational expert

Sunday, 29 December 2013

Operesheni Tokomeza Ujangili Haifanani na Sobibor



Wapenzi waperuzaji wa blogu yetu, natumaini mmesherehekea vema sikukuu ya Krismasi na kuelekea mwaka mpya. Kwa kuwa nimekuwa kimya kitambo kidogo si vema kama sitagusia kutoa salamu za pole kwa msiba wa Shujaa Nelson Mandela. Hii inatokana na kuwa nje ya ofisi kwa kipindi cha wiki tatu hivi. Kama nilivyoandika katika ukurasa wetu wa facebook nampenda Thatha Mandela kwa jambo kubwa moja “ alifungwa gerezani kwa miaka ishirini na saba, katika kipindi hicho alijifunza kusamehe na si kulipa kisasi” kama dunia ingepata watu kama Mandela wenye moyo wa kusamehe hakika bara letu lisingekuwa na migogoro mingi ya kisiasa kwani yote chanzo chake ni ubinafsi na visasi. Kwa kuwa hiyo si habari yangu mahsusi kwa leo acha niifanye ya akiba ili kuruhusu makala ya leo.
Mwishoni mwa mwaka tumeshuhudia simanzi kubwa ikiibuliwa nchini baada ya kusomwa kwa ripoti Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira kuhusu Operesheni Tokomeza Ujangili. Nimejitahidi sana kujizuia nisiandike chochote juu ya  Operesheni Tokomeza Ujangili lakini ghafla nikajiwa na kumbukumbu mbaya za maangamizi ya wayahudi miaka ya 1940 kwenye kambi SOBIBOR mpakani mwa Ujerumani na Poland. Operesheni iliyoongozwa na dikteta Aldolf Hitler ama tunaweza kuyaita maangamizi ya karne iliutisha ulimwengu, Ulaya hata Ujerumani yenyewe, ni mauaji yaliyoambatana na mateso makali pamoja na matumizi ya gesi yenye sumu. Ndugu zangu Sobibor ilitisha kwani vijana wenye nguvu walifanyishwa kazi ngumu zenye mateso makali hata kufia kazini, watoto na wazee waliingizwa kwenye tanuru la moto na kuchomwa humo. Maangamizi haya ya wayahudi wengi wasio na hatia yalifanywa na askari wa Ujerumani kwa amri ya amiri jeshi mkuu wao Aldof Hitler katika kipindi cha vita ya pili ya Dunia.
Ndugu zangu nimeanza kwa kugusia tukio la kutisha la SOBIBOR baada ya kutafakari ripoti ya Lembeli na kupata mrejesho mbalimbali kutoka kwa wabunge na watanzania. Ninajaribu kuitofautisha Operesheni tokomeza Ujangili na maangamizi ya wayahudi kwa kuwa ni kama vinafanana. Ndio kwani Operesheni hii askari walipohojiwa walisema wanatekeleza agizo la Amiri Jeshi mkuu wakati Ujerumani pia ilikuwa kutii agizo la Amiri jeshi Mkuu dikteta Adolf Hitler, Operesheni Tokomeza Ujangili ilifanywa na jeshi la ulinzi na jeshi la polisi kadhalika maangamizi ya wayahudi.
Pamoja na ufanano huo lakini nimebaini tofauti kubwa ya ile operesheni ya Hitler na hii ya vijana wa Mh. Kikwete. Wakati ile ya Hitler ilitokana na chuki juu ya ustawi wa Wayahudi kwetu Tanzania haikuwa hivyo bali ilikuwa chuki ya askari kwa watanzania tofauti pasipo kujali rangi wala kabila, kila waliyemkumba walimuona ni jangili hata kama anauza nyanya. Ukatili wa Operesheni hii ni mbaya haijawahi tokea, kwani ni zaidi ya vita maana nijuavyo katika vita husikika milio ya risasi askari huua ili kusonga mbele. Lakini katika Operesheni hii askari walipiga kambi katika vijiji wakakamata watu na kuanza kuwadhalilisha, udhalilishaji wa hali ya juu, wengine waliwatesa ili mradi vurumai. Hapo ndo huwa nachanganyikiwa kwamba askari hawa walikuwa na chuki na nani na kwa sababu gani? Wajipambanue kwani Ujerumani walijitambulisha wazi kuwa walikuwa na chuki na wayahudi. Sielewi kama taaluma yao ina mapungufu makubwa hata kutoweza kubaini wahalifu hivyo kuamua kusomba kila waliyemuona, na hata walipoamua kuwasomba je hawaelewi katiba inasemaje juu yao? Hakuna mahakama hata wakageuka wao askari na tena mahakimu wakiwahukumu watu kwa adhabu kali hata kuwaua? Je askari hawa walikuwa wanatekeleza agizo la nani? Maana amiri jeshi mkuu Mh Rais Kikwete hakusikika akiagiza wakaue, wakadhalilishe na kuwatesa watanzania au labda kwa kuwa waziri Kagasheki alisema ikiwezekana majangali yauawe hukohuko?
Jaman watanzania tumefikia huko? Sasa nababaika ikiwa wanajeshi wanaoiwakilisha nchi huko Lebanon, Sudani na Kongo kama wanatuwakilisha vema kwani ikiwa watanzania wenzao wanawatenda hivi je hao wa huko si mara mia? Hebu tuangalie sehemu ya ripoti inapoonyesha udhalilishaji uliotokea.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, James Lembeli akisoma ripoti hiyo bungeni alisema Operesheni Tokomeza Ujangili, ulisababisha hofu miongoni mwa wananchi na viongozi na baadhi yao kuyakimbia makazi. Lembeli alisema watuhumiwa, walikamatwa, walipekuliwa na  kudhalilishwa na baadhi kutojulikana walipo.
“Baadhi ya wananchi wakiwemo viongozi, madiwani na wenyeviti wa vijiji na vitongoji na watumishi wa Serikali, walikamatwa na kudhalilishwa mbele ya wananchi wanaowaongoza,” alisema Lembeli
Aliongeza; “Watuhumiwa waliokamatwa walidai kudhalilishwa mbele ya wanafamilia kwa kupewa adhabu wakiwa uchi na wanawake kushikwa sehemu za siri bila ridhaa yao.”
Lembeli alitoa mfano kuwa Ali Nyenge (38) wa Kata ya Iputi, Wilaya ya Ulanga alidai kuvuliwa nguo, kumwagiwa maji yaliyochanganywa na chumvi na kuchapwa viboko huku mwanawe wa kiume (11) akishuhudia huku akilazimishwa kuchora picha ya Chatu kwa kutumia wembe kwenye paja lake.
Alisema mwanamke mmoja wa  Babati (jina tunalo) alidai kuvuliwa nguo na kulazimishwa kufanya mapenzi na wakwe zake, pia kuingizwa chupa sehemu zake za siri.
Aidha, baadhi ya wanawake walidai kubakwa na kulawitiwa huku wilayani Ulanga, mwanamke mmoja alidai kubakwa na Askari wawili wa Operesheni Tokomeza Ujangili mida ya usiku.
Hivi kama Operesheni hiyo ingeendelea japo kwa mwaka mmoja ingekuwaje? Si ni zaidi ya SOBIBOR maana ya Hitler hatukusikia ubakaji, kulazimisha wakwe kufanya mapenzi, hatukusikia uingizaji wa chupa, kujichora kwa nyembe mwilini na mateso mengi kama yaliyofanywa katika operesheni hiyo. Hakika haifanani hata kidogo.
Hebu tazama baadhi ya picha na video zikionyesha sehemu ya Operesheni hiyo;

Hii ndio moja ya unyama uliofanyika kwenye Operation Tokomeza Ujangili iliyosimamiwa na washiriki toka Wizara 4 za mawaziri waliondolewa juzi bungeni.

Hapa raia wakiadhibiwa vikali na askari walioendesha Operesheni hiyo.

tazama video kwa mujibu wa youtube.com pia imechapihwa na http://jumamtanda.blogspot.com/2013/12/video-inayodaiwa-watuhumiwa-wa-ujangili.html
Japo ripoti hiyo imesababisha mawaziri wanne kutenguliwa uteuzi wao lakini kwa nchi yetu ambayo inaiangaza Afrika na Dunia nzima kwa mwenge wake juu ya Mlima Kilimanjaro, inatupasa kwenda mbali kuwakabili wote waliojaribu kuichafua nchi yetu waliothubutu kuondoa amani kwa raia wasio na hatia. Kila aliyehusika katika operesheni hiyo si tu afukuzwe kazi kuwafuata wakubwa zake mawaziri waliofukuzwa,  la hasha wataendelea kutamba mtaani bali wakamatwe wapelekwe mahakamani wakashtakiwe ili wajue ni nchi inayoendeshwa kwa mujibu wa katiba na si wahuni na wababe wachache.
Hapa natamani kuzichochea taasisi zinazoweza kusisitiza haki kutendeka, yaani vyama vya siasa, tume ya haki za binadamu na wanaharakati mbalimbali kupaza sauti zao katika hili kwani likipita kimya kwa kuwawajibisha mawaziri tu linaweza kujirudia na kuwa baya zaidi.
Wahenga walisema Hala hala Mti na Jicho.

No comments:

Post a Comment