m
"If you want to conquer fear, don't sit at home and think about it. Go out and get busy. "
-- Dale Carnegie, motivational expert
Wednesday, 12 October 2016
Rais Magufuli aagiza viongozi walioalikwa kuhudhuria sherehe za mwenge kutohudhuria, awataka warudishe posho.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameagiza viongozi wote wa Serikali walioalikwa kuhudhuria sherehe za Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa zitakazofanyika tarehe 14 Oktoba, 2016 katika Wilaya ya Bariadi Mkoani Simiyu kutohudhuria sherehe hizo na wale ambao walishalipwa fedha ya posho na safari kwa ajili hiyo wazirejeshe
Taarifa iliyotolewa leo tarehe 12 Oktoba, 2016 Ikulu Jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi imeeleza kuwa Rais Magufuli ametoa maagizo hayo ikiwa ni utekelezaji wa azma ya Serikali ya awamu ya tano ya kubana matumizi yasiyo ya lazima na kuelekeza rasilimali nyingi katika shughuli za maendeleo ya nchi.
Viongozi waliotajwa kutakiwa kufuta safari zao za kwenda Bariadi ni pamoja na Wakuu wote wa Mikoa, Wakuu wote wa Wilaya, Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mameya na Wenyeviti wote wa Halmashauri za Majiji, Manispaa, Miji na Wilaya pamoja na watumishi ambao huambatana nao wakiwemo madereva na wasaidizi wao ambao kwa idadi hufikia takribani 1,500.
Kwa kuwa sherehe za Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru huambatana na Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Muasisi wa Taifa na Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyefariki dunia miaka 17 iliyopita, agizo hilo limewataka Viongozi wote wa Mikoa na Wilaya kubaki katika maeneo yao ya kazi na kujiwekea utaratibu wa jinsi ya kuienzi siku hiyo.
Aidha, Rais Magufuli ameagiza Wilaya zote ambazo zimefanya vizuri katika shughuli za maendeleo wakati Mwenge ulipokuwa katika maeneo yao, zitambuliwe kwa kutangazwa rasmi katika siku ya kilele cha Mbio za Mwenge na kwamba zawadi zilizoandaliwa zitapelekwa kwa wahusika kwa utaratibu utakaoelekezwa na Mamlaka inayohusika kutoa zawadi hizo.
Hata hivyo Dkt. Magufuli ameelekeza kuwa kutokana na umuhimu wa Mwenge wa Uhuru kwa Taifa, Viongozi wote wa Serikali ya Mkoa wa Simiyu na Wilaya zake pamoja na wananchi wote wa mkoa huo wajitokeze kwa wingi na kushiriki katika sherehe za kuzima Mwenge wa Uhuru siku hiyo ya tarehe 14 Oktoba, 2016.
Mgeni Rasmi katika sherehe za kuzima Mwenge wa Uhuru atakuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein.
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
Tuesday, 11 October 2016
Angela Merkel azindua Jumba la makao makuu ya AU lililopewa Jina la Julius Nyerere, Addis Ababa.
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel
amezindua jumba jipya makao makuu ya Umoja wa Afrika ambalo limepewa
jina la rais mwanzilishi wa taifa la Tanzania, Julius Nyerere.
Jumba hilo ambalo jina lake kamili ni Jumba la Amani na Usalama la Julius Nyerere limejengwa kwa ufadhili kutoka Ujerumani.
Litakuwa
makao ya idara ya Amani na Usalama ya AU na litatumiwa pia na maafisa
wa kutoa tahadhari ya mapema kuhusu mizozo barani pamoja na kuratibu
juhudi za kulinda amani za AU.
Ujenzi wa jumba hilo, ambalo ukubwa
wake wa sakafu ni mita 13,500 mraba na linaweza kutumiwa na wafanyakazi
360, uligharimu euro 27 milioni.
Jumba hilo afisi za kufanyia
kazi, vyumba vya mikutano vya kutumiwa na Baraza la Amani na Usalama,
chumba cha kuratibia shughuli, maktaba na vyumba vya shughuli za
pembeni.
Mwalimu Nyerere, ambaye alikuwa rais wa Tanzania hadi
1985, alikuwa mmoja wa viongozi waanzilishi wa Muungano wa Nchi za
Afrika (OAU) ambao sasa ni Umoja wa Afrika (AU).
Alishiriki sana katika jitihada za kuendeleza bara
la Afrika na kusaidia mataifa ambayo hayakuwa yamepata uhuru kujipatia
uhuru wake.
Mwalimu Nyerere alipigania sana kumalizwa kwa ubabe wa
Wazungu katika nchi za Rhodesia (sasa Zimbabwe), Afrika Kusini, na
taifa la Kusini Magharibi mwa Afrika/Namibia (sasa Namibia).
Source:BBCSwahili
Subscribe to:
Posts (Atom)