Kwa ufupi
- Kwa kipindi kirefu msitu huo umekuwa eneo la kufanyia mauaji kwa watu wasio na hatia, ambapo genge la wahalifu kutoka Kenya limedaiwa kuhusika na mauaji hayo.
Matukio ya mauaji ndani ya msitu wa Mwakijembe
yameendelea kutishia usalama wa Watanzania, wanaoishi jirani na eneo la
Horohoro linalopakana na nchi jirani ya Kenya.
Kwa kipindi kirefu msitu huo umekuwa eneo la
kufanyia mauaji kwa watu wasio na hatia, ambapo genge la wahalifu kutoka
Kenya limedaiwa kuhusika na mauaji hayo.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini
msitu huo wenye rasilimali nyingi unaodaiwa kutumiwa na genge hilo kwa
vitendo haramu vya ujangili, uchimbaji madini na uvunaji wa miti,
ikiwemo uchomaji mkaa.
Taarifa za uchunguzi ambazo zilithibitishwa na
viongozi wa Serikali ya Vijiji vinavyopakana na msitu huo, zilibaini
genge hilo limekuwa likiua kila linayemhisi atafichua uhalifu wao.
Inatoka UK 1
Uchapisha wa Hati za Kusafiria (Kwa mujibu wa
taarifa za karibuni, kwa mwaka huu pekee, watu wawili tayari wameshauawa
kwa kuchinjwa ndani ya msitu huo.
Matukio hayo ya mauaji yalithibitishwa na Diwani
wa Kata ya Mwakijembe, Ramadhani Mtiota ambaye alisema kwa sasa katika
eneo hilo hali imekuwa ya hofu kutokana na kuongezeka kwa makundi ya
vijana wa rika la Morani wa Kimasai, wanaojiandaa kuvishambulia vijiji
vya Kenya.
Diwani huyo alisema ametoa taarifa kwa Mkuu wa
Wilaya ya Mkinga, Mboni Mgaza kuhusu hali hiyo pamoja na Mwenyekiti wa
Halmashauri ya Wilaya hiyo, Andrew Ngoda.
Hata hivyo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tanga,
Constantine Massawe alisema wanafahamu kuhusu mauaji yanayotokea kwenye
msitu huo.
Alisema taarifa za mauaji ya hivi karibuni ya watu
wawili, Ali Mohamed na msichana wa kabila la Kimasai Kendie Minja
yanafahamika na yanafanyiwa uchunguzi na polisi.
”Ninachofahamu ni mauaji yaliyofanyika ya msichana
Kendie kuchinjwa na kufichwa msituni upande wa Kenya, lakini upelelezi
unafanywa na Jeshi la Polisi la wenzetu wa Kenya kwa hivyo sijui zaidi
ya hivyo,” alisema Massawe.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mkinga, Mboni
Mgaza alisema anaandaa mkutano wa ujirani mwema utakaowahusisha viongozi
wa Serikali Mkoa wa Tanga na Jimbo la Mombasa, Kenya.
http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/Mauaji-ya-kutisha-yaibuka-msituni/-/1597296/1869732/-/11tcb6hz/-/index.html
http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/Mauaji-ya-kutisha-yaibuka-msituni/-/1597296/1869732/-/11tcb6hz/-/index.html