Waziri Mkuu wa Japani Shinzo Abe Jumamosi (01.06.2013) ameahidi kutowa
msaada wa dola bilioni 32 kwa Afrika katika kipindi cha miaka mitano
kusaidia ukuaji wa uchumi wa bara hilo kupitia sekta za serikali na
binafsi.
Waziri Mkuu wa Japani Shinzo Abe ametoa ahadi ya masaada huo wakati wa
ufunguzi wa mkutano wa kimataifa wa siku tatu kuhusu maendeleo ya Afrika
unaofanyika katika mji wa Yokohama nchini Japani.
Msaada huo unajumuisha utowaji wa yeni bilioni 650 kwa ajili ya mikopo
katika ujenzi wa miundo mbinu na mpango wa mafunzo kwa ajili ya vijana
wa Afrika.Mpango huo utawapa fursa vijana 1,000 wa Kiafrika kujifunza
katika vyuo vikuu vya Japani na kujifunza kazi katika makampuni ya
Kijapani.
Abe amesema kuendeleza rasilmali ya nguvu kazi, huduma muhimu za
matibabu na kukuza sekta ya kilimo ni mambo muhimu katika kuchochea
ukuaji wa uchumi wa Afrika.Amesema kile inachokihitaji Afrika ni
uwekezaji katika sekta ya binafsi ambapo ushirikiano kati ya sekta za
umma na binafsi utatoa fursa ya kufaidikia na uwekezaji huo. #
Shauku ya Japani kuwekeza Afrika
Waziri Mkuu wa Japani Shinzo Abe wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa
Kimataifa wa Maendeleo ya Afrika (TICAD) mjini Yokohama Japani.
Tangazo lake hilo linaonyesha shauku ya Japani kuchuana na
China katika masuala ya kuipatia msaada na kuwekeza Afrika bara lenye
utajiri wa mali asili.
Licha ya uhusiano wa muda mrefu uliopo kati ya Japani na Afrika,umuhimu
wa Japani kwa bara hilo umekuwa ukipunguwa kulinganishwa na ule wa China
ambapo kiwango chake cha biashara na Afrika ikilinganishwa na Japani ni
mara tano zaidi na mara nane zaidi katika uwekezaji wa moja kwa moja.
China huwa haitangazi kiwango cha msaada wake wa maendeleo lakini repoti
zinadokeza kwamba hutoa hadi dola bilioni mbili kila mwaka.Kiwango
ilichotangaza Japani Jumamosi kimepita sana kiwango hicho cha
China.Uhusiano wa Japani kwa Afrika unatofautiana na mataifa mengine kwa
bara hilo amesema Abe katika kauli inayoonekana kuikusudia China.
Serikali ya China imekuwa ikishutumiwa na baadhi ya nchi kwa kile mara
nyengine kinachoonekana kuwa inachofanya barani humo ni kunyakua ardhi
na kutohusisha uwekezaji na masharti ya kuboresha haki za binaadamu au
kuzitaka nchi zinazopokea misaada kuwa wazi zaidi.
Waziri Mkuu huyo wa Japani amesema mali asili ya Afrika inasababisha
kuwepo kwa fursa muhimu za biashara kwa nchi yenye uhaba mkubwa wa mali
ghafi kama Japani lakini nchi hiyo haitotafuta na kuchimba rasilmali
hizo kwa sababu tu ya kuzileta Japani.
Msaada ukuze uchumi
Waziri Mkuu wa Ethiopia Hailemariam Desalegn na Waziri Mkuu wa
Japani Shinzo Abe wakati wa ufunguzi wa mkutano wa TICAD mjini Yokohama
Japani.
Amesema wataisaidia Afrika ili kwamba mali asili za Afrika
zisababishe ukuaji wa kiuchumi wa bara hilo.Abe pia ametoa wito wa
kuanzishwa kwa kanuni za uwazi katika biashara na kuimarisha usalama kwa
Wajapani wanaoishi na kufanya kazi barani Afrika.Waziri Mkuu wa
Ethiopia Hailemariam Desalegn ameitaka Japani kuimarisha uwepo wake
barani Afrika.
Akizungumza katika kikao cha ufunguzi wa mkutano huo wa Kimataita wa
Tokyo kuhusu Maendeleo ya Afrika (TICAD), amesema ni jambo la kushangaza
kwamba kuhusika kwa Japani katika fani ya uwekezaji barani humo kuko
nyuma kabisa kuliko vile ingelipaswa iwe kwa hivi sasa kulinganisha na
nchi mpya ambazo hivi sasa zimekuwa zikijihusisha katika harakati
nyingi.
Afrika lazima ibadilike
Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini.
Suala la uwekezaji katika sekta ya binafsi limekaribishwa na
wajumbe ambapo Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini amesema uchumi wa bara
hilo hauna budi kuendelezwa. Amesema Afrika lazima ibadilike kutoka kuwa
na uchumi unaotegemea usafirishaji nje wa bidhaa na kuwa na uchumi
wenye kuongozwa na viwanda pamoja na kutanuwa njia mbali mbali za
kiuchumi.Zuma amesema mambo matatu ni muhimu kufikia maendeleo nayo ni :
kuunganisha masoko, kuendeleza viwanda na kuendeleza miundo mbinu.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon pia amehudhuria mkutano huo
ambapo amesema malengo ya mkutano huo ni malengo ya Umoja wa
Mataifa.Amesema wamejizatiti kuisaidia Afrika itimize Malengo ya
Maendeleo ya Milenia yakiwemo kutokomeza umaskini na njaa ifikapo mwaka
2015.
Mkutano huo wa TICAD utaendelea kufanyika hadi Jumatatu ambapo wajumbe
kutoka zaidi ya nchi 50 za Afrika watakuwa wanajadili na Japani jinsi ya
kuhakikisha ukuaji wa uchumi endelevu barani Afrika.Mkutano huo
unaandaliwa kwa ushirikiano wa mashirika ya kimataifa kama vile Umoja wa
Mataifa,Benki ya Dunia na kwa mara ya kwanza Umoja wa Afrika.Mkutano
huo umekuwa ukifanyika kila baada ya miaka mitano nchini Japani tokea
ulipoanzishwa hapo mwaka 1993.
Mwandishi : Mohamed Dahman/AFP,dpa
Mhariri :Caro Robdw
dw.de