m

"If you want to conquer fear, don't sit at home and think about it. Go out and get busy. "

-- Dale Carnegie, motivational expert

Monday, 4 March 2013

Matokeo mabovu na Umuhimu wa FDC



Matokeo ya kidato cha nne kwa mara nyingine yamekuwa mabaya na mabaya zaidi ukilinganisha miaka mingine, wengine wameyaita bomu japo binafsi sioni kama ni bomu nahisi ni moshi tu mlipuko wenyewe bado. Naeleza hivi kwa sababu bado kuna kila dalili ya bomu lenyewe yaani tutegemee matokeo mabaya zaidi ikiwa hatua hazitachukuliwa. Ukirejelea makala yangu ya mwaka jana (2012) yenye kichwa Unahitajika Utafiti wa Kina Juu ya Ufaulu wa Wanafunzi inayopatikana http://kapagiii.blogspot.com/search?updated-min=2012-03-01T00:00:00-08:00&updated-max=2012-04-01T00:00:00-07:00&max-results=2 ilieleza wazi walengwa sita wanaopaswa kutazamwa juu ya matokeo ya kidato cha nne. Nitawaorodhesha kwa ufupi uwezo wa wanafunzi wenyewe (personal ability), Mzazi wa mwanafunzi, mwalimumazingira ya elimu na shule zenyewe, jamii yote kwa ujumla na mwisho serikali na vyombo vyake muhimu vya elimu, wizara, Taasisi ya Elimu Tanzania.
Nasikitika kuwa matokeo ya mwaka 2011 licha ubovu wake hakuna utafiti wowote hata ripoti ya nini kilisababisha na matokeo yake ndo haya matokeo yenye kuvunja rekodi. Nashukuru sasa kumeundwa tume, nikitazama wajumbe wa tume napata tumaini ninapoona jina la Rakesh Rajan katibu mtendaji wa Twaweza ambao wanajihusisha sana na utafiti wa elimu ukiwemo ule wenye kichwa “Are Our Children Learning” wa mwaka 2010 ambao binafsi nilipousoma nilibaini matatizo makubwa katika elimu yetu lakini cha ajabu utafiti wako haukutiliwa mkazo na serikali yetu. Serikali yetu ni bingwa wa kutupa mafaili ya utafiti na ripoti mbalimbali pasipo kujali gharama na faida yake. Prof. Kezilahabi katika riwaya yake ya “Nagona” ya mwaka 1978 anajaribu kueleza hili anapoonyesha mafaili ya utafiti yakiwa yametupwa jaani. Chonde ripoti itakayopatikana kutokana na tume hii itendewe kazi ikiwa tunataka kuliokoa Taifa hili la sivyo bomu kubwa litapuka.
Pamoja na matokeo hayo binafsi nakumbuka umuhimu wa vyuo vya maendeleo ya jamii (FDC) na vyuo vya ufundi. Kundi hili kubwa la watoto waliofeli cha kusikitisha ni kuwa haliwezi kujitegemea na hivyo kama tungekuwa na vyuo vya maendeleo ya jamii na hata vya ufundi vya kutosha vingesaidia kupunguza mzigo huu. Inasikitisha kuona vyuo hivyo havikuendelezwa na hata vilivyopo vipo katika hali mbaya, kwa mifano hai unaweza kutembelea FDC- Katumba(Tukuyu), FDC-Bigwa (Morogoro), FDC- Uyole (Mbeya) na FDC-Kibaha (Pwani) vyote vinatapatapa katika hali mbaya kabisa. Kama kundi hili lililofeli halitapatiwa ujuzi wowote litaleta shida baadaye kwani hata Johannesburg ule mji wa pili kwa uhalifu duniani umesababishwa na vijana waliokosa tumaini la maisha baada ya kukosa elimu. Japo elimu hii ya ufundi inadharauliwa lakini ikumbukwe kuwa ndiyo iliyowakomboa wachina na sasa wanatamba maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Nimalize kwa kusisitiza serikali kuchukua hatua za maksudi katika elimu na pia kuangalia vyuo vya maendeleo ya jamii na vyuo vya ufundi ili watoto wanapofeli wasiachwe tu bali wapate elimu ya ufundi, na wanafunzi wawe tayari kuipata ikiwa ni pamoja na wazazi kutoa ushirikiano wa dhati. Kwa pamoja tunaweza kuikomboa nchi yetu.
Wenu
Peter Kapagi
SJUT-Dar es Salaam
Simu ya kiganjani;    +255 764 734620
Baruapepe;     kakakapagi@gmail.com       Blogu;             www.kapagiii.blogspot.com