Tanzania inajitayarisha kupeleka majeshi katika Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ili kupambana na Kikundi cha Machi 23 (M23)
kinachopigana kuiangusha serikali ya Kongo, maafisa wa Tanzania
waliiambia Sabahi.
Majeshi ya Tanzania yatapelekwa kama sehemu ya misheni ya kulinda
amani chini ya mamlaka ya Umoja wa Mataifa, njia hiyo hiyo ambayo
wamekuwa wakipelekwa katika nchi nyingine katika eneo hilo. Msemaji wa
jeshi la Ulinzi la Tanzania Kanali Kapambala Mgawe alisema siku ya
Ijumaa (tarehe 30 Novemba).
"Tanzania imekuwa ikijihusisha na misheni za amani, mafunzo na
ushauri kwa nchi nyingi," aliiambia Sabahi, na kueleza kuwa majeshi ya
Tanzania yamekuweko katika misheni hizo huko Lebanoni, Darfur, Sudani ya
Kusini, Visiwa vya Komoro na Liberia.
"Tanzania daima haiendi kwa nchi yeyote bila ya kuombwa na nchi hiyo au kutoka Umoja wa Mataifa," alisema.
Mgawe alisema kuwa kwa vile mzozo wa DRC hauna tishio lolote maalumu
kwa Tanzania, viongozi wa kikanda wanazidi kuwa na wasiwasi kuwa hali ya
kutokuwepo kwa utulivu unaoweza kusababishwa.
Mataifa wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa
Afrika (SADC) wanafanyakzi pamoja ili kuhakikisha kuwa serikali za
kidemokrasia katika eneo hilo hazitishiwi au kuangushwa na waasi, na
kwamba utawala wa sheria ndio utakaotawala, alisema.
M23 kiliundwa tarehe 4 Aprili mwaka huu na takriban askari 300
walioigeuka serikali ya DRC, wakitaja hali duni jeshini na kutokuwa
tayari kwa serikali kuwatekeleza makubaliano ya amani ya tarehe 23 Machi
2009, makaubaliano ambayo yamekipatia jina kikundi hicho.
M23 pia kimemshutumu Raisi wa DRC Joseph Kabila kwa kufanya
udanganyifu katika uchaguzi wa Novemba 2011, ambao uchaguzi uligubikwa
na upinzani wa vurugu, kuenea kwa matatizo ya vifaa na ukosolewaji wa
kimataifa.
Mazungumzo ya amani yenye nguvu
Kutekwa kwa mji wa Goma na M23 hapo tarehe 20 Novemba, mji mkuu wenye
utajiri wa rasilimali katika Mkoa wa kaskazini wa Kivu, miezi minane
baada ya kuanzisha uasi wao dhidi ya serikali, kulizua hofu ya vita
vipana zaidi na matatizo makubwa ya kibinadamu, shirika la habari la AFP
liliripoti.
Kukindi hicho kilijitoa kutoka Goma siku ya Jumatatu (tarehe 3
Disemba), ingawaje wapiganaji wake wamebaki karibu na mji na bado
hawajarejea nyuma kilomita 20 zilizokubaliwa katika mazungumzo ya
kikanda.
Kiongozi wa kisiasa wa M23 Jean-Marie Runiga alisema siku ya Jumanne kuwa kikundi chake kilikuwa tayari kuzungumza na serikali.
Mazungumzo yataanza "siku chache zijazo mjini Kampala", Waziri wa
mambo ya Ndani wa DRC Richard Muyej Mangez alithibitisha. Alisema kuwa
serikali itapeleka kikosi kamili wakiwemo viongozi muhimu wa kijamii na
wajumbe wa bunge la taifa na seneti.
Hata hivyo, Kabila -- ambaye kikundi cha M23 kimemtaka awachie ngazi
toka madarakani -- hakitarajiwi kuhudhuria katika mazungumzo ya awali.
Wakati huo huo, wataalamu wa Umoja wa Mataifa walitoa kile
walichosema kuwa ni ushahidi moya ambao "unashikilia imara" shutuma za
mwanzo kuwa Rwanda na Uganda viliwasaidia M23.
Ripoti hiyo ambayo AFP iliipata siku ya Jumatatu, inasema kuwa Rwanda
na Uganda zilikisaidia M23 katika mashambulizi yake, huku Uganda ikitoa
msaada wa vifaa na mama ya majeshi ya Rwanda kujiunga na kikosi ambacho
kiliuteka Goma.
Rwanda na Uganda zilikataa katakata kuhusika katika mzozo huo.
Walinda amani wanajiandaa
Wakati taharuki iko juu, Tanzania inaendelea na mipango yake ya
kupeleka kikosi kimoja chenye askari kati ya 700 na 800 chini ya
uangalizi wa SADC, ikisubiri amri ya Umoja wa Mataifa, Waziri wa Mambo
ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa wa Tanzania Bernard Membe alisema.
Mwezi Agosti, nchi wanachama 11 za Mkutano wa Kimataifa juu ya Eneo
la Maziwa Makuu (ICGRL) uliomba SADC kupeleka askari 4,000 huko DRC
baada ya kuthibitishwa na Kifungu cha 7 cha mamlaka ya Umoja wa Mataifa,
inayowapa walinda amani mamlaka ya kuchukua hatua iwapo raia watakuwa
katika tishio la mara moja.
Mpaka sasa, Umoja wa Mataifa umeruhusu tu walinda amani kujilinda
wenyewe iwapo watashambuliwa chini ya Kifungu cha 6 cha mamlaka yake,
ambacho hakiruhusu kuwa na wajibu zaidi ya huo.
"Tunalaani kile waasi wanachofanya huko mashariki mwa Kongo," Membe
alisema. "Haikubaliki kwa Tanzania." Ili kuimarisha amani katika DRC,
majeshi yanaweza kutumia nguvu ili kutekeleza majukumu yao, alisema.
"Tanzania inawataka waasi waondoke Goma na maeneo mengine muhimu
wanayoshikilia ili kuruhusu mazungumzo, au Umoja wa Mataifa utatoa
kibali kwa majeshi ya SADC kuwa sehemu ya misheni ya kuyasaidia majeshi
ya serikali ya DRC mara moja," alisema.
Vitisho kwa Tanzania
Mzozo wa DRC ni muhimu kwa Tanzania kwa sababu ikiwa utaachwa bila ya
kuangaliwa, utakuwa na athari za kijamii na kisiasa kwa mataifa
wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Membe alisema. Tanzania
inaweza kukabiliwa na kumiminika kwa wingi kwa wakimbizi ikiwa mzozo
utaenea, na kulifanya taifa kuwa katika hatari sana kwa vitisho vya
usalama, alisema.
Tanzania imekuwa ikiwapokea wakimbizi kutoka Burundi na DRC tangu
miaka ya mwanzo ya 1990. Hadi kufikia mwezi Januari huu, kulikuwa na
zaidi ya wakimbizi 130,000 nchini, nusu yao wakitokea DRC, kwa mujibu wa
Kamishna wa Umoja wa Mataifa kwa Wakimbizi.
Membe alisema kuwa wadau wa kanda lazima waonyeshe uongozi na kufuata mkabala wa kuwa wenye harakati ili kutuliza hali.
Mnamo tarehe 24 Novemba, Raisi Jakaya Kikwete alikutana na Kabila,
Raisi wa Uganda Yoweri Museveni, Raisi wa Kenya Mwai Kibaki na
mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika Nkosazana Dlamini-Zuma katika
mkutano wa tano wa ICGRL.
ICGRL ilitoa wito kwa M23 kusitisha shughuli zote za vita, na
kuzitaka pande zote mbili za M23 na serikali kufungamana na makubaliana
yaliyotangulia. Washiriki kwa mkutano huo pia walitoa wito kwa nchi za
eneo hilo kuchukua wajibu mkubwa zaidi wa kuhakikisha amani ya DRC.
Hatua za wananchi
Wananchi jijini Dar es Salaam walieleza maoni tofauti kuhusu ama
Tanzania ingejishughulisha katika operesheni ya kijeshi huko DRC.
Omary Mkonge, mwenye umri wa miaka 75, alisema anapingana na serikali
kupeleka askari huko DRC. "Hakuna haja kwetu kuingilia kati katika vita
hivi na vitaigharimu sana nchi yetu," alisema. "Unaona, miaka 33 baada
ya vita na Uganda, nchi yetu bado haijatengamaa kiuchumi. Bado tuna
makovu ya vita."
Mkonge alisema kuwa serikali inapaswa kutumia nyenzo zake ili
kuwasaidia Watanzania, baadhi yao wanaoshi katika umasikini wa kutisha.
Kambarage Manuga, mwenye umri wa miaka 80, yeye alisifia uamuzi wa
Tanzania kupeleka wanajeshi kuwalinda wale ambao wako katika hatari ya
kuathirika haraka.
"Katika vita vyovyote, kutokana na uzoefu wangu mrefu, wanawake,
watoto na wazee ndio wanaoteseka zaidi," aliiambia Sabahi. "Ninaunga
mkono hatua hiyo ya serikali yangu kuingilia kati mzozo wa DRC. Huwezi
kubakia katika amani ambapo nyumba ya jirani yako inaungua moto
Chanzo;Mwananchi