Kitendawili
cha Kuchinja Nyama Nchini Tanzania
Ndugu Mtanzania
kwa miezi kadhaa sasa kumekuwepo na mvutano mkubwa juu ya uchinjani nyama chini
Tanzania, yaani nani mwenye haki ya kuchinja kati ya muislamu na mkristo.
Mvutano huo umepelekea mgogoro kule Geita na sasa Tunduma. Jambo hili limekuwa KITENDAWILI maana
kinahitaji jibu na mwenye kutupa jibu hatuna hakika kama analo au la maana yupo
kimya. Binafsi ninao mtazamo juu ya jambo hili na ningependa kuchangia. Kwanza
ningependa kueleza ukweli usiojulikana kwa wengi yaani kwa wakristo walio wengi
na pengine waislamu na wapagani pia. Nauita ukweli usiojulikana kutokana na
kwamba baada ya mvutano huo kutokea nikajaribu kuhojiana na watu kadhaa juu ya
jambo hili, ajabu ni kuwa walio wengi walionekana kutofahamu lolote juu ya
machinjio yetu nchini, mmiliki na hata mchinjaji halali. NCHINI TANZANIA MACHINJIO HALALI KISHERIA YANAMILIKWA NA HALMASHAURI ZA
MIJI NA WACHINJAJI HALALI NI WAISLAMU. Kwa upeo mdogo nilionao ni kwamba
kwa muislamu mnyama aliyechinjwa na mtu asiye muislamu au pasipo swala basi
nyama hiyo itakuwa kibudu(nyama haramu). Kwa mkristo ninajua jambo moja kwamba
damu iliyomwagika msalabani ina nguvu ya kutakasa na zaidi wamepewa mamlaka ya
kukanyaga ng’e na nyoka tena kula vitu vya kufisha na kwamba havitawafisha
kabisa, tena wameambiwa wafanikiwe katika katika mambo yote na kuwa na afya
njema kama roho ifanikiwavyo(Marko 16:16-18,
3Yohana 1:2).
Ninavyoelewa ni
kwamba serikali yetu ina tamka wazi kuwa haina dini lakini inasisitiza
kuheshimu imani kwa kila mtu. Ni jambo jema kabisa kwa serikali ambayo ina watu
wa dini tofauti tena kwa makundi makubwa kujitenga na dini ili kila mtu awe
huru kuabudu anachotaka. Zipo nchi nyingi za kidini (Non secular states) kama
Saudi Arabia na hata Uingereza kwani yenyewe inajihusisha zaidi na kanisa lake
la Anglikana. Swali langu ni kwamba serikali yetu nzuri inayotamka wazi haina
dini imewezaje kutumia kigezo cha dini katika machinjio yake? Inawezaje kuamini
kwamba muislamu ndiye halali kuchicha na si mkristo wakati yenyewe haina dini?
Ninachofahamu ni kuwa serikali ilijitenga na dini si kuruhusu tu uhuru wa
kuabudu chochote kwa watu wake bali pia kuondoa migogoro ya kidini. Mtu
akijifanya kuficha tone la mafuta ndani ya maji litaelea tu! Na sasa ndo hilo
linaelea baada ya kufichwa kwa miaka mingi na limekuwa kitendawili na jibu lake
lahitaji mji.
Kama
kitendawili hiki ningetegewa mimi ningejibu hivi; serikali haina dini na kwa
kuwa machinjio ni ya serikali basi iamue pia kutokuwa na dini hata katika
machinjio, yaani iajiri wachinjaji pasipo kufuata imani awe muislamu, mkristo
na hata mpagani maana serikali yetu inawatambua, si wapo wabunge waioapa kwa
korani wala Biblia Takatifu? Suala la dua, swala, maombi au maombezi ya nyama
yabakie kwa mlaji, mlaji baada ya kununua nyama awajibike kuitakasa ili iwe
halali sawa na imani yake. La sivyo serikali ijitenge na machinjio jambo ambalo
ni hatari zaidi kwani ni vigumu kutenga nchi nzima machinjio ya wakristo,
waislamu, wahindu, wapagani na watu wa imani nyinginezo maana zipo nyingi.
Ikitenga machinjio itabidi itenge na mabucha na hapo ndo utakuwa mwanzo wa
ubaguzi wa kidini.
Naishauri
serikali kuchukua hatua za haraka juu ya jambo hili ili kuepuka majuto.
Huu ni mtazamo
wangu, si wa dhehebu wala dini yangu.
Wako katika
safari,
Mwl Peter
Kapagi