Wapenzi wangu leo nipo tena ili
kukushirikisha katika habari zetu KII. Kama ujuavyo moto wetu ni “habari ni
Maisha” kumbe ukikosa habari huna maisha na ukipata habari njema utakuwa na
maisha mema na ukipata habari mbaya ni matokeo ya maisha mabaya. Kilichopo
mezani leo ni juu ya vijana wenzangu na mpango unaopaswa kuwasaidia vijana.
Ndugu zangu sina mpango wowote unaoweza
kuwasaidia vijana lakini nafikiri kwamba ni stahiki sana kuwa na mpango huo
kama tunalitakia mema Taifa letu. Kumekuwa na ongezeko la vijana nchini, katika
ongezeko hilo kuna kundi kubwa la vijana wasio na elimu wala ajira na kundi la
pili ni lile lililo katika mfumo wa elimu na hata kupata elimu lakini likiwa na
wasiwasi wa ajira. Ongezeko hilo ndio linalonitia wasiwasi na hatima ya Taifa
letu hivyo kunisukuma kuandika makala haya.
Kabla sijaendelea naomba nigusie uhalifu
katika majiji makubwa na yanayoongoza kwa uhalifu duniani, nazungumzia Paris
–ufaransa Rio De Jeneiro- Brazil na Johannesburg- Afrika kusini. Ndio majiji
hatari zaidi duniani kwa uhalifu lakini swali la kujiuliza ni nani wanaofanya
uhalifu huo? Na kwanini? Kwa haraka utagundua kuwa majiji hayo ndio yale yenye
vijana wengi waliokosa ajira. Katika majiji hayo matatu utabaini zaidi kuwa
majiji mawili ni yale yenye mgogoro wa ubaguzi wa rangi. Sitaki kuzungumzia
sana ubaguzi wa rangi bali nataka kugusia ubaguzi na mipango mibovu kwa vijana
katika maendeleo ya Taifa lolote duniani Tanzania ikiwa mfano. Afrika kusini
ilikumbwa na ubaguzi wa rangi na katika ubaguzi huo uligusa pia elimu na ajira
pasipo kujali athari itakayopata baadaye. Hali kadhalika Paris ilikumbwa na
wahamiaji haramu wa Afrika kaskazini hasa kutoka nchi za Algeria na makoloni
yake kama Senegal. Wahamiaji wakaingia
nchini ufaransa na wenyewe wakawaadhibu si tu kuwafukuza bali hata waliobaki
kwa kuwabagua kama wasio na haki nchini humo. Athari yake ndio yanayowapata
sasa kwani wale vijana waliobaguliwa na kunyimwa elimu au ajira sasa wamegeuka
kuwa wahalifu kama njia yao ya kujikimu na maisha.
Unapoamua kuwa mbaguzi lazima ujitenge
kabisa jamii ile unayoibagua na ikiwa umeamua kuishi nayo ni lazima ukatae
ubaguzi kwa gharama zote, huwezi kumbagua siku zote mtu unayeishi naye mahali
pamoja.
Nchi yetu sasa ina ongezeko kubwa la
vijana wasomi na wasio wasomi bila kuwepo na mipango madhubuti ya kuwasaidia kukabili changamoto ya ajira.
Watawala hujisahau sana kuhusu vijana kwani huona wao na familia zao wako
salama hakuna tatizo lolote kwani hata ajira zimekuwa kwa kibendera. Hakuna
mipango ya makusudi ya kuwasaidia vijana
katika ajira na ukizingatia mfumo wetu wa elimu unamuandaa kijana kuwa afisa wa
kukaa ofisini tu, mfumo wa elimu ya kikoloni ili wakoloni kujipatia maofisa
wachache katika ofisi zao kuendelea kuwatawala waafrika. Kuna haja ya kuwepo
kwa mipango ya namna vijana wanavyoweza kutengeneza ajira mbali ya
kung’ang’ania zile za serikali na mashirika kwani tayari kuna wasomi wengi kwa
ngazi ya sekondari, astashahada, stashahada hadi shahada wasio na ajira na bado
wana matumaini ya kuajiriwa. Wana matumaini makubwa kila watazamapo vyeti vyao
lakini ukweli ni kwamba hakuna ajira nchi hii tupilia mbali zile chache
ziwatoshao wenyewe. Nchi isiyo na viwanda, isiyo na miundombinu ya afya na
elimu haiwezi kuwa na ajira za kutosha kwani wataalamu ambao wangeajiriwa
kwenye hospitali, shule, vyuo, migodini na viwandani itawalazimu kubaki
wakirandaranda mitaaani wakiwa na matumaini ya ajira ilhali hakuna ajira.
Mpango niutakao ni kuwabadili vijana
wasifikiri juu ya njia moja ya ajira yaani kutegemea kuajiriwa badala yake
kujiaajiri, wafunzwe kwamba ajira ni pamoja na kujiajiri na hata kutengeneza ajira kwa ajira kwa ajiri
ya wengine. Serikali inapaswa kufanya mambo mawili muhimu kubadili mtazamo wa
vijana katika ajira na pili ni kuwasafishia njia ya kujiajiri. Binafsi sioni
njia bora ya kujiajiri katika nchi zaidi ya viwanda na kilimo ndio nafasi
zinazopaswa kupewa kipaumbele. Nchi ya Tanzania bado haijawa ya kiviwanda na
wala sioni kama ni nchi ya kilimo inababaika tu lakini tunaweza kuleta mageuzi
na mageuzi yoyote huletwa na vijana hata uhuru wa Afrika uliletwa na vijana
machachari akina Kwame Nkrumah, Mwl. J.K Nyerere, komredi R. Mugabe na
wengineo. Tugeukie viwanda kwani nchi yetu ina matumizi makubwa kabisa ya
bidhaa za viwandani lakini ajabu ni kwamba asilimia kubwa ya bidhaa hutoka nje
ya nchi. Kama ni elimu tayari tunayo japo viwanda vingine havihitaji elimu,
kwani ni elimu gani inahitajika ili kutengeneza vijiti vya meno (Toothstick),
Kalamu, rula, chaki n.k mbona navyo vyatoka nje? Ni dhahiri kuwa kama
vingetengenezwa nchini tungetengeneza ajira kwa vijana wengi kabisa.
Inashangaza kuona nchi bado inategemea bidhaa ndogondogo za nyumbani kama
sabuni, sukari, chumvi, kutoka nje ya nchi na watanzania wakiona fahari kutumia
bidhaa za nje kuliko za ndani. Binafsi nimekuwa nikitoa semina za ujasiriamali
ninapopata nafasi ya kufanya hivyo katika pitapita yangu katika mitandao ni
mebaini kuna mitambo ya hadi milioni 8 na hata ya chini ya hapo inayoweza kuchonga
bidhaa ndogondogo kama mishumaa, vijiti vya meno na kutengeneza chaki ni
mitambo rahisi isiyohitaji elimu kubwa. Mbali ya hivyo serikali iliyoweza
kuwashawishi wenye viwanda kutoka nje kama kiwanda cha Nation kilichokuwa
kinazalisha betri na redio za nation inashindwaje leo kuwashawishi Wajapan,
wachina na wahindi kuleta viwanda vyao nchini ili tusiendelee kuagiza bidhaa za
kielekroniki kama redio, ngamizi, simu na magari wakati sisi ni wateja wao
wakubwa? Sijui wizara inayohusika na viwanda inafanya nini kuhusu hili na wizara
inayohusika na ajira inaishauri nini wizara ya viwanda? Kama hakutakuwa na
hatua za makusudi kuongeza viwanda vidogo na vya kati ajira itaendelea kuwa
tatizo kubwa na mfumuko wa bei utakuwa donda ndugu katika nchi yetu kwani tumekuwa
na matumizi makubwa ya fedha za kigeni kuliko uzalishaji.
Katika kilimo bado hatujaamua kukifanya
kuwa uti wa mgongo wa uchumi wa nchi yetu na hatimaye kutengeneza ajira. Kwetu
kilimo imebakia kuwa sekta ya walalahoi na watu waliokosa elimu, fikra potofu
kabisa. Hebu tazama pamoja na kuwepo kwa mapori mengi bado nchi imekuwa na
tatizo kubwa la chakula katika mikoa ya Shinyanga, Singida na Dodoma. Maana
yake mahitaji ya chakula yamekuwa makubwa kuliko uzalishaji wakati huohuo kukiwa
na tatizo la ajira. Watu hawana la kufanya wakati mapori yanakaa bure na
mahitaji ya chakula ni makubwa. Ni ajira ngapi tupata kama tukamua kuzalisha
chakula cha kutosheleza mahitaji yetu potelea mbali kuzalisha kwa ajili ya
kuuza nje ya nchi ambako pia kuna mahitaji makubwa ya chakula? Ajabu zaidi hata
matunda yanatoka Afrika ya Kusini kwa mfano Tufaha maarufu kama apple huagizwa
kutoka Afrika ya kusini ingawa yanastawi maeneo ya baridi kama Iringa na
Njombe. Kuna haja gani ya kunywa maziwa ya Kenya ili hali tuna mamilioni ya ng’ombe
nchini? Nina maswali mengi yakisubiri majibu.
China tuionayo leo hatukuwa na tofauti
sana tulipokuwa tunapata uhuru, imestawi
sana baada kujihakikishia kwanza soko la ndani la bidhaa zake yaani wananchi
wake yenyewe, wakafanya uzalishalishaji mkubwa ndipo kutanua uchumi wake na
kuweza kushindana na mataifa makubwa kiuchumi. Nasi tuna soko letu la ndani
kwani watu milioni arobaini na uchee si haba. Tukizalisha kwa ajili yetu tu
tutaiimarisha shilingi yetu na hatimaye kuwa na uchumi unaostawi lakini vijana
wakipata utulivu kwa ajira kemkem.
Tazama utengenezaji wa vijiti vya meno
Picha za mashine rahisi za kutengeneza vijiti na mishumaa
Lazima uandaliwe mpango kwa ajili ya
vijana na kupata mustakabali wa baadaye
wa kwao wenyewe vijana na Taifa letu. Kama haitafanyika hivyo nchi hii haiitakuwa
salama tena kwani wasionacho watapopoteza matumaini utakuwa mwanzo wa uhalifu
mkubwa kwa walionacho. Hatuna tofauti na nchi za Ufaransa na Afrika Kusini
kwani hata elimu yetu ni ya kibaguzi kwa sehemu kwani wenye nacho wanapata elimu bora kuliko
wasionacho na katika ajira vivyo hivyo.
Hata hivyo ninatoa rai kwa vijana kuwa
tayari kwa ajili ya ajira yoyote yenye kuingiza kipato wawe tayari kutumia
uwezo wao wote kubuni ajira ili kuleta mageuzi kama tukitaka ajira za serikali
tu nchi yetu itaangamia na katika kuangamia huko athari kubwa ni kwa makabwela
kama siye.
Wako
katika safari
Ndg.
Peter Kapagi 09.01.2014
Mbeya