TAKWIMU ZAONYESHA TANGU MWAKA 1985-2012 MAKANISA 46 YAMECHOMWA ,KUBOMOLEWA NCHINI
![]() |
Askofu David Mwasota. |
Imeelezwa
kuwa tangu kuibuka kwa wimbi la uchomaji
wa makanisa linalofanywa na watu
wanaoaminika kuwa wanaharakati wa
Kiislamu katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limeyakumba zaidi ya
makanisa 46.
Hayo
yameelezwa na Katibu Mkuu wa Baraza la
Maaskofu wa Kipentekoste nchini Tanzania (PCT) Askofu David Mwasota wakati
akizungumza na Gazeti Msemakweli akiwa Kisiwani Zanzibar.
Kiongozi
huyo alikuwa mmoja wa wajumbe wa mkutano uliowakutanisha viongozi wa dini
ya Kikristo, viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ)na makamanda
wakuu wa jeshi la Polisi ambapo ulijadili kwa kina juu ya vurugu zilizotokea
visiwani Zanzibar.
Kwa
mujibu ya Mwenyejiti wa kundi linaloendesha mihadhara ya Kikristo
inayosahihisha upotoshwaji wa Maandiko Matakatifu ya Biblia unaofanywa na
Wahadhiri wa Kiislamu Mwinjilisti Cecil Simbaulanga, takwimu zinaonesha kwamba makanisa yaliyoteketezwa na Waislamu tangu
mwaka 1985 visiwani Zanzibar pekee ni
26, huku Tanzania Bara yakifikia 20.
Askofu
Mwasota alisema hadi mapema wiki
iliyopita wanaharakati wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu
Zanzibar(JUMIKI) walipofanya vuruguru na kuchoma moto makanisa kisiwani Zanzibar, viongozi wa
Kikristo wamekuwa wakitoa taarifa za
uhalifu dhidi ya makanisa na nyumba za wachungaji, lakini hakuna hatua
zilizochukuliwa.
Katika
mahojiano kwa njia ya simu na Msemakweli, Askofu Mwasota alisema kutokana na
hilo, viongozi wa Kikristo waliokutana na viongozi wa SMZ katika Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG) Kariakoo
lililochomwa moto, alisema kimsingi viongozi hao kupitia Waziri wa Nchi Ofisi
ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Bwana Mohammed Aboud Mohammed, waliahidi kuyalinda makanisa dhidi ya Waislamu
wakorofi.
''Angalau
kauli kama hiyo imetupa moyo na
kuturidhisha kwa vile haikuwepo siku za nyuma na kweli tunashuhudia ulinzi umeimrishwa makanisani”, alisema Askofu
huyo wakati akihojiwa na Msemakweli kwa njia ya simu kutoka Zanzibar.
Alisema
tayari watu 30 wamekamatwa kuhusiana na vurugu hizo.
Hata
hivyo alipoulizwa nini serikali inasema
kilikuwa chanzo cha vurugu hizo, alisema bado uchunguzi unaendelea na
kwamba si vyema kukurupuka na kutaja
chanzo hicho kabla ya uchunguzi makini kufanyika.
Kwa
upande wake Waziri wa Mambo ya Ndani Dakta Emanuel Nchimbi aliyeshiriki katika
mkutano huo, alionya kuwa suala la amani
na ulinzi wa raia na mali zao halina
mjadala na kuvitahadharisha vikundi vinavyohatarisha amani na kwamba vitapambana na mkono wa Dola.
Mei
26 na 27 mwaka huu, vurugu kubwa zilitokea kisiwani Zanzibar
baada ya wafuasi wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu
Zanzibar (JUMIKI), kushinikiza Jeshi la Polisi limuachie kiongozi wao
Sheikh Mussa Issa ambaye alikamatwa.
Baada
ya wafuasi hao kushindwa kuvamia kituo cha Polisi Madema, kufuatia Askari wa
FFU kuwatawanya kwa mabomu ya machozi, waliamua kuingia mitaani na kufanya
kitendo cha kushangaza cha kuharibu mali za makanisa mawili na
kuyachoma moto.
Katika
kile kinachooneka kuwa nyuma ya vurugu
hizo kuna mkono wa udini na siasa, licha ya wafuasi wa JUMIKI kuchoma moto
makanisa, pia walikuwa wakiwasaka watu kutoka Tanzania Bara huku wakitamka kwamba hawautaki muungano.
Wakati
kanisa
la TAG lilichomwa moto Mei 27 mwaka huu, Porikia ya Kanisa Katoliki
Mpandae iliripotiwa kuchomwa moto mchana wa Mei 28 mwaka huu na kundi
la
wafuasi wa JUMIKI lililokuwa likitoka katika Mahakama ya Mwanakwerekwe
kusikiliza kesi ya wenzao waliokamatwa kwa kuhusika na vurugu hizo.
Kati
ya watu 30 waliokamatwa na kufikishwa mahakamani wamo viongozi watatu wa JUMIKI akiwemo mkuu wake
Sheikh Mussa Juma Issa, ambapo wanatuhumiwa
kukusanyika kinyume na sheria na kufanya fujo. Watuhumiwa hao hata hivyo wako
nje kwa dhamana.
Naye
Mwenyekiti wa Kundi la Biblia ni Jibu nchini Tanzania
ambalo ni maarufu kwa kupigania imani ya Kikristo dhidi ya upotoshwaji unaofanywa
na Wahadhiri wa Kiislamu Cecil Simbaulanga aliliambia Msemakweli kuwa vurugu
za Zanzibar ni
za kidini dhidi ya Ukristo.
“Ndio
maana waliohusika ni nazo ni Mashehe wanaoeneza chuki dhidi ya Ukristo. Haya yote
nilishayaeleza katika katika kitabu
changu kinachozungumzia Mchango wa Kanisa katika miaka hamsini ya Uhuru, ambapo
katika ukurasa wa 36 niliitaka serikali kuchukua hatua za kudhibiti wimbi la
uchomaji makanisa”, alisema Simbaulanga.
Alisema
kwa kilichotokea sasa anaitaka serikali
ya Jamhuri ya Muungano na ile ya Mapinduzi ya Zanzibar ifidie makanisa sita yaliyochomwa moto
katika vurugu za sasa kutokana na uzembe
wake na kutosikiliza hoja za maana.
“Unajua
haiingii akilini kwamba Waislamu Zanzibar ambao ni asilimia 99.9 inakuwaje
walalimikie mfumo Kristo”, alisema Mwinjilisti Simbaulanga na kubainisha kuwa
kinachofanyika ni mbinu tu za kusambaza chuki ili kuua Ukristo Zanzibar.
Alisema
kwa hali ilivyo sasa ni lazima SMZ iache kufundisha watoto Uislamu pekee
katika shule za msingi kama inavyofanya sasa, Kama
kweli inataka haki itendeke.
Mwinjilisti
Simbaulanga alilitaka Jeshi la Polisi na SMZ kutopotosha ukweli kwamba
wanaofanya vurugu za uchomaji moto makanisa ni wahuni bali waeleze ukweli
kwamba ni Waislamu.
“Haya
mambo sisi tunajua. Tunazo DVD za wote waliopanga mambo haya kuanzia mwanzoni
mwa mwaka huu, kama
ushahidi mzito na tunawajua. Tuko tayari kutoa ushahidi huo.Hawa sio wahuni ni
viongozi wa wanaharakati wa Kiislamu wanaofahamika wazi”, alisisitiza
Simbaulanga.
Akizungumza
na Msemakweli Mwenyekiti wa Umoja wa Wainjilisti wa Kikristo nchini Tanzania
(UWAKITA) Mwinjilisti Samson Bulegi ambaye pia ni Mwenyekiti wa kundi la Injili
kwa Wote ambalo moja ya shughuli zake ni kusahihisha upotoshaji wa imani ya
Kikristo unaofanywa na makundi ya Wahadhiri wa kiislamu, alisema vuguru za Zanzibar kwa sehemu kubwa
zina mkono wa dini na siasa.
Alisema
kisiasa JUMIKI na makundi mengine ya wanaharakati wa Kiislamu hayataki Muungano
kwa vile Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa uhuru wa kuabudu
ambao unakwamisha juhudi zao za kuunda dola la Kiislamu.
“Wanataka
muungano
uvunjike ili wapate fursa ya kueneza Uislamu na kuua Ukristo na ndio
maana hawawataki watu wa bara, huku pia wakichoma moto makanisa”,
alisema
Bulegi.
Alisema
kuwa Muungano unasababisha watu kutoka Bara kuingia kwa wingi Zanzibar kuhubiri Injii na kufungua makanisa;
hali inayosababisha Waislamu wengi kuokoka
na kuwa Wakristo,
“Unajua mambo ndivyo yalivyo. Hata Makamu wa
kwanza wa Rais wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ya Zanzibar Sheikh Maalim Seif
Sharif Hamad, aliwahi kukiri kwamba
Wakristo wanabaguliwa Zanzibar.
Mimi naiomba SMZ kukomesha jambo hili
kwani kila mtu ana haki ya kuishi kwa uhuru bila kubaguliwa”, alisema Bulegi.
“Bila kukomesha ubaguzi huu na unyanyasaji wa
Wakristo, moto utawaka na kusambaa kila mahali na hali kuwa mbaya zaidi”,
alitahadharisha Bulegi.