Kibali
ni hali ya kukubalika, kuthibitika(approval) na kuwa na Baraka na fadhila za
pekee katika maisha. Na kutafuta kibali ni hali ya kuhitaji kupata kukubalika,
kuthibitika na kupata Baraka na fadhila za pekee katika maisha. Kibali kina
uhusiano wa karibu na huruma na neema.
Kupata
kibali kwa Mungu na Bwana wetu Yesu Kristo kunategemea ridhaa(Pleasure) ya Mungu
mwenyewe na kinaweza kuongezwa(extended) kwa kuishi kwa haki na maombi. Kwa
hiyo tunaona kuwa kibali kinaweza kuja moja kwa moja yaani mtu anazaliwa nacho
lakini pia maisha ya haki au utakatifu na maombi yanaweza kumwezesha mwamini
kupata kibali. Kwa mfano Musa (Kutoka 33:12-13) alizaliwa na kibali hata pale
alipotupwa majini bado alionekana na si kwa watu masikini lakini watu wakubwa
kabisa katika nchi, kibali chake hakikuweza kuzuiwa na mtu yeyote katika maisha
yake, na hata mauti ilipata kibali kiasi cha kuzikwa na Mungu Mwenyewe…kutembea
na kibali ni raha sana, na kama utaweza kujifunza kwa watu kadhaa katika biblia
waliopata na kutembea na kibali hutachoka kuisoma Biblia, hutaichoka imani yako
na hautachoka kuomba maana moyo wote utavutwa kuhitaji kibali cha Mungu.
Kupata
kibali ni jambo moja na kutembea katika kibali ni jambo lingine, unaweza
kuzaliwa na kibali cha Mungu lakini usitembee katika kibali hicho isipokuwa kwa
uhitaji wa kibali, maombi na bidii ya kutafuta kibali. Kwa kweli kutafuta kibali
ni jambo la msingi kwa mwamini kwani linaleta raha ya wokovu na wepesi wa
msalaba na hivyo kuchochea imani na bidii ya utakatifu. Kibali kinalipa katika
maisha, kwa mfano Yusufu na Danieli walipata uwaziri mkuu si kwa vigezo wala
uwezo bali kwa kibali pekee, Daudi alipata Ufalme sababu alitembea katika
kibali, Nehemia aliweza kujenga ukuta wa Yerusalemu uliobomoka kwa sababu ya
Kibali, Esta naye akawa Malikia katika nchi ya utumwa kwa sababu ya kibali.
Kibali ni kwa ajili ya huduma yako, kibali ni kwa ajili ya kazi, masomo,
uongozi, na maisha yako yako ya kila siku, kibali ni ushindi wako, na jamaa
zako. Ukipata kibali hakika hata ndugu zako watafaidi, majirani wataoga katika
baraka zako na kila eneo utakalokuwepo litanufaika kwa wewe kutembea katika kibali.
Kwa hiyo kutotembea katika kibali si kwamba unajinyima mwenyewe bali unawanyima
haki hata ndugu, majirani na wafanyakazi wenzako kwani Bwana anataka kutupa
kibali kwa ajili yetu na wengine, tukisoma Mwanzo 12:2 inasema …nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na
kukubariki, na kulikuza jina lako, nawe uwe Baraka( maana yake ufanyike
Baraka kwa wengine).
Tunza kibali na tembea katika kibali.
Kupoteza kibali ni kupoteza kila kitu.
Hebu
tupitie watumishi wa Mungu waliofaidi na kufurahia kutembea katika kibali cha
Mungu;
1.
Yusufu,
kwa kweli namuona ndiye mtu aliyepata kibali cha pekee (Supernatural favor) kwa
kuyatazama maisha ya Yusufu kuzaliwa, kuuzwa, kuishi gerezani, kuwa waziri mkuu
na kuwafadhili wana wa Israeli wakati wa njaa (Mwanzo sura ya 37-50), tukisoma
mwanzo 39:1-5 …5Mbaraka wa
Bwana ukawa juu ya vyote alivyokuwa navyo katika nyumba…
2.
Abram/Ibrahimu,
huyu ndio aliahidiwa kubarikiwa hadi uzao wake. Neno lenyewe latosha kueleza
kibali chake kwa wakati Mwanzo 12:2 Bwana anamuahidi Kibali Ibrahim Mwanzo 13:2
inathibitisha kibali na kwamba alitembea katika kibali naye Abraham alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha na kwa
dhahabu pia sura ya 24:1 inasema b Bwana alikuwa amembariki
Ibrahimu katika vitu vyote.
3.
Daudi,
hata simba na dubu walitambua kibali chake lakini kibali chake hakikuonekana
hadi alipofanya kazi ya kumwua Goliathi. 1Samweli 18:6-7
...Sauli ameua elfu zake,
Na Daudi kumi elfu zake.
Wanawake waliimba hivyo na
kuthibitisha kibali cha Daudi kuliko Sauli. Daudi alitembea na kibali tangu akiwa
kijana hadi ufalme, hata ufalme wake ulipata ushindi kwa kila vita.
4.
Danieli;
Nabii aliyeishi utumwani Babeli lakini kwa kibali cha Mungu hata kupata uwaziri
mkuu wakati hakuwa na kigezo chochote cha kushika wadhifa wa juu Babeli.
Danieli 1:9 Basi Mungu akamjalia Danieli
kupata kibali na huruma machoni pa huyo mkuu wa matowashi. 6:3 basi Danieli huyo alipata sifa kuliko
wakubwa na maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake(ni roho ya
kibali), naye mfalime akaazimu kumweka
juu ya ufalme wote.
5.
Esta,
Naye kama Daniel alikuwa katika nchi ya ugeni akilelewa na Mordekai mara wazazi
wake walipofariki, pamoja na kuwa mateka lakini alifanikiwa kuingia katika
mashindano ya kutamfuta malkia wa mfalme Ahasuero na akashinda (Esta 2:5-17) mstari wa 15b unasema naye huyu Esta alikuwa amepata kibali
machoni pa wote waliomwona. Na 17 inaongeza mfalme akampenda Esta kuliko wanawake wote, naye akapata neema na
kibali machoni pake kuliko mabikira wote. Utaona kuwa Esta alikuwa na
kibali ambacho kikamwezesha kukubalika na hata kuthibitika mbele ya watu wote na
mfalme. Tangu zamani hata leo mfumo wa utawala hauruhusu mtu asiye mzawa
kushika nafasi ya juu ya uongozi lakini Esta alifanikiwa tena akapendwa kuliko
wanawake wote. Kibali kinafanya mtu apendwe mahali popote na watu wote, kibali
kinamfanya mtu awe na mvuto wa sura, maongezi na kazi yoyote afanyayo. Kibali
ni raha sana kwa mwamini, naweza kusema ukitembea na kibali utaishi popote na
kwa nafasi ya pekee.
Muda huu wa ibada moja hautaweza
kutosha kama tutataja watu wote waliotembea katika kibali cha Mungu… lakini ni
vyema kujua ni muhimu kutafuta kibali kwa Mungu na kutembea katika kibali
hicho.
Unaweza kupata kibali kwa
maombi kama Musa alivyoomba neema (Mwanzo 33:12-13) na Neno linasema katika
Zaburi 84:11 Kwa kuwa Bwana Mungu ni jua
na ngao, Bwana atatoa neema na utukufu. Hatawanyima kitu chema hao waendao kwa
ukamilifu. Kuna jambo lingine linaloweza kumpatia mtu kibali ambalo ni Ukamilifu, kuishi maisha makamilifu ya
haki na utakatifu.
Pia kibali yaani
kukubalika na hata kuthibitika kunaweza kupatikana kwa uaminifu na huduma
njema, Yusufu alipata kibali kwa Potifa kwa sababu alitawala vizuri nyumba
yake… ni kweli alizaliwa na kibali lakini kilithibitika kwa kuwa mwaminifu na
bidii ya kazi kwa Potifa. Ruthu alitafuta kibali kwa mumewe Boazi kwa kumfanyia
ukarimu mkwewe Naomi(Ruthu 2:2). Na Na hata Daudi kibali chake kilianza
kuonekana mpaka pale alipojitosa kumpiga Goliathi.
Mwamini
yeyote asimame kwa miguu yake mwenyewe aombe kibali kwa mungu kwa ajili ya kila
jambo… ukipata kibali hakuna jambo litakalokwama. Kibali ni kwa ajili yako,
kazi yako, majirani zako, ndugu zako na zaidi kwa jili ya utukufu wa Mungu.
Isaya 60:1
Ondoka uangaze kwa kuwa nuru
yako imekuja,
Na utukufu wa Bwana umekuzukia
Godbless you servant of God have been blessed.
ReplyDelete